Na ASP. Lucas Mboje, Dodoma.

GEREZA Kuu Isanga, Dodoma leo limepokea msaada wa vifaa mbalimbali vilivyotolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulia Kazi, Vijana na Ajira Mhe. Anthony Mavunde (Mb) kwa ajili ya kusaidia kupambana na janga la Corona magerezani.

Akizungumza jijini Dodoma mara baada ya kupokelewa kwa msaada huo uliojumuisha sabuni, ndoo za maji pamoja na  vitakasa mikono(Sanitizer), Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Suleiman Mzee amemshukuru Naibu Waziri Mavunde pamoja na Wadau mbalimbali wa Jeshi hilo wenye nia njema ambao wanaendelea kujitokeza kuunga mkono jitihada za Serikali katika kukabiliana na janga la corona nchini.

“Mhe. Mavunde nikushukuru sana kwa msaada wa vifaa hivyo ulivyovikabidhi leo katika Gereza Kuu la Isanga, Dodoma kwani vitasaidia maafisa, askari pamoja na wafungwa na mahabusu katika kujikinga na corona magerezani”, alisema Kamishna Jenerali Suleiman Mzee.

Akikabidhi msaada huo wa vifaa, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulia Kazi, Vijana na Ajira Mhe. Anthony Mavunde (Mb) alimuahidi Kamishna Jenerali wa Magereza nchini kwamba huo ni mwanzo na yuko tayari wakati wowote kutoa mchango wake pale itakapohitajika kufanya hivyo.

Wakati huo huo, Gereza hilo mapema leo limepokea msaada wa vifaa mbalimbali vya kibinadamu kwa ajili ya wafungwa na mahabusu vyenye thamani ya Shilingi Milioni 5,500,000/= ambavyo vimetolewa kwa pamoja na MTANDAO wa Watumishi wa Umma Wanawake ujulikanao kama Viongozi Wanawake Wanaoibukia Tanzania(Emerging Women Leaders in Tanzania – EWLT).

Kufuatia kuripotiwa uwepo wa ugonjwa wa corona(COVID -19) nchini, Jeshi la Magereza Tanzania Bara limeendelea kuchukua hatua za tahadhari ikiwemo kusitisha kwa huduma zote za kutembelea wafungwa na mahabusu pamoja na kuletewa chakula mahabusu waliopo magerezani. Aidha, Jeshi hilo linaendelea kuchukua tahadhari na hatua kwa kadri litakavyoona inafaa sambamba na kuzingatia miongozo mbalimbali inayotolewa na Serikali dhidi ya janga hilo. Kwa habari picha Zaidi bofya hapa